
Mbunge wa kigoma
kaskazini(CHADEMA),Naibu katibu Mkuu wa Chadema,Naibu kiongozi wa kambi
ya upinzani Bungeni, na Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi,Mheshimiwa
Zitto Kabwe
---
I. UTANGULIZI
Mheshimiwa
Spika, kwa niaba ya Kambi ya Upinzani, ninatoa maoni ya Kambi ya
Upinzani kuhusu Bajeti ya Nchi ya mwaka wa fedha 2012/2013 kwa mujibu wa
Kanuni za Bunge Kifungu cha 99(7) toleo la Mwaka 2007.
Mheshimiwa
Spika, Natoa pongezi za dhati kabisa kwa Ndugu William Augustao Mgimwa,
Mbunge wa Jimbo la Kalenga mkoani Iringa kwa kuteuliwa na Rais kuwa
Waziri wa Fedha na Uchumi. Vile vile nawapongeza Ndugu Saada Mkuya na
Ndugu Janeth Mbene kwa kuteuliwa kwao kuwa Wabunge na baadaye kuwa
Manaibu Mawaziri katika Wizara hii nyeti sana. Ninawapa pole pia maana
Wizara ya Fedha sio Wizara lelemama. Kambi ya Upinzani itaendelea
kuisimamia Wizara hii kwa ukaribu sana kama ilivyofanya katika kipindi
cha miaka miwili iliyopita. Mtakapofanya vizuri tutawapongeza ili
muongeze juhudi, mtakapoharibu tutawawajibisha.
Mheshimiwa
Spika, Ni dhahiri kwamba Mwaka wa Fedha uliopita ulikuwa mwaka mgumu
sana kwa Watanzania. Ni mwaka ambao gharama za maisha zilipanda kwa kasi
kubwa sana na juhudi za Serikali kuwakwamua wananchi na hasa wananchi
wanyonge kutoka kwenye lindi la ufukara ziligonga mwamba. Kambi ya
Upinzani inawapa pole Watanzania kwani hili ndilo walilochagua. Muhimu
ni kuvumilia mpaka uchaguzi ujao na kufanya mabadiliko ya Serikali ili
kuweka Serikali itakayoongozwa na CHADEMA na itakayoweza kukabili
changamoto za sasa na za baadaye.
Mheshimiwa Spika, naomba tufanye mapitio kidogo ya Bajeti inayomaliza muda wake.
UTEKELEZAJI WA BAJETI ILIYOPITA
Mheshimiwa
Spika, kabla ya kutoa bajeti mbadala ya Kambi ya Upinzani ni vema
kufanya tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya Serikali iliyopita ili
kuona ni kwa namna gani Serikali inathamini fedha za walipa kodi, na
dhamira yake ya kuleta maendeleo ya kiuchumi katika Taifa. Katika
kufanya hivyo, tutapitia baadhi ya maeneo ambayo Kambi ya Upinzani
tunaona kuwa hayakutekelezwa katika bajeti iliyopita.
Kupunguza Makali ya Maisha
Mheshimiwa
Spika, Katika Bajeti ya mwaka 2011/12 Serikali ilitangaza nia yake ya
kupunguza makali ya maisha. Hatua mbali mbali zilichukuliwa ikiwamo
kupunguza kodi na tozo kwenye mafuta ya Dizeli na Petroli, kuanza
kutekeleza mpango wa dharura wa umeme na kutoa fedha za kununua chakula
kwa Wakala wa Chakula. Serikali ilitumia shilingi bilioni 296 na dola za
Marekani milioni 183 kwenye Umeme. Vilevile Serikali ilitumia shilingi
bilioni 27 kununua Mahindi na kusambaza kwenye masoko.
Mheshimiwa
Spika, licha ya hatua hizo zilizochukuliwa Mfumuko wa Bei uliongezeka
maradufu kutoka wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2010/11 mpaka wastani wa
asilimia 17.8 mwaka 2011/12. Serikali imefeli katika lengo lake la
kupunguza makali ya maisha kwa wananchi. Sio tu kwamba Serikali
imeshindwa kudhibiti upandaji holela wa gharama za maisha bali pia hatua
za Serikali zimeongeza kasi ya kupanda kwa makali ya maisha.
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani Bungeni katika Hotuba yake mbadala ya mwaka
2011/12 iliitaka Serikali kushughulikia msingi wa mfumuko wa Bei hapa
nchini ambao ni uzalishaji mdogo wa mazao ya chakula. Tumeelezwa na
Waziri Kivuli wa Mipango na Uchumi kwamba Chakula peke yake ni asilimia
48 ya kapu la bidhaa na huduma ambazo mwanachi anatumia. Mfumuko wa Bei
ya Chakula kinacholiwa nyumbani na kwenye migahawa ilikuwa asilimia 25
mwezi Aprili 2012 (BoT monthly Economic Review, May 2012). Vile vile
mfumuko wa bei wa nishati inayotumika nyumbani na mafuta ya Dizeli na
Petroli ulifikia asilimia 25 pia mwezi Mei mwaka 2012. Ni dhahiri kwamba
iwapo tutadhibiti mfumuko wa bei ya chakula tutaweza kushusha mfumuko
wa bei kurudi kwenye tarakimu moja.
KUSOMA HOTUBAYOTE YA MSEMAJI
MKUU WA KAMBI YA UPINZANI BUNGENI NDUGU KABWE ZUBERI ZITTO (MB), WIZARA
YA FEDHA NA UCHUMI, KUHUSU MAPENDEKEZO YA MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA SERIKALI KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013 BOFYA HAPA NA ENDELEA..
0 comments:
Post a Comment