Wakimbizi 480,000 warejeshwa Burundi
Wakimbizi 480,000 raia wa Burundi waliokuwa wakiishi katika makambi ya Mishamo na Katumba yaliyoko wilayani Mpanda na Ulyankulu mkoani Tabora, wamerudishwa kwao tangu zoezi la kuwarejesha kuanza mwaka 2002.
Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha, ilisema katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, serikali ya Marekani imewapokea wakimbizi 12,000 raia wa Burundi waliokuwa wakiishi nchini na sasa wanaishi Marekani ikiwa ni makubaliano ya kimataifa ya kuhamisha wakimbizi katika nchi tatu.
Taarifa hiyo ilifafanua kuwa wakimbizi 100,000 wamepewa uraia wa Tanzania na wametakiwa kuhama maeneo yao ya awali waliokuwa wakiishi na kuungana na jamii ya Watanzania katika maeneo mengine.
Taarifa hiyo pia ilisema Waziri Masha ameiomba Jumuiya ya Kimataifa kutoa misaada kwa wakimbizi hao waliopewa uraia ili kuuwaanzishia maisha mapya.
Mpaka sasa kuna jumla ya wakimbizi 150,000 wanaosubiri kurejeshwa Burundi mwishoni mwa mwaka huu, kwa mujibu wa taarifa hiyo.
0 comments:
Post a Comment