Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amepiga marufuku hospitali, zahanati na vituo vya afya vya serikali kujengwa maeneo ya mabondeni na juu ya milima ili kulinda usalama wa majengo.
Katika tamko la serikali lilisomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa Wilaya ya Temeke, Hellen Mcha kwenye maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Upunguzaji wa Maafa, Waziri Mkuu Pinda alisema vyombo hivyo vya kutoa huduma ya afya ni muhimu kujengwa katika maeneo salama.
Alisema wakati maafa yanapotokea, watu walioathirika wanatakiwa kufikishwa hospitali na vituo vya afya kwa ajili ya kuokoa maisha yao na endapo vituo hivyo vitakua vimeharibika, maisha yao yatakuwa hatarini kwa kukosa huduma.
Waziri Mkuu Pinda alieleza licha ya watu kukosa huduma ya afya, pia wagonjwa waliolazwa na watumishi wanaathirika.
Waziri Mkuu, alitolea mfano tetemeko la ardhi liloharibu vituo vya kutolea huduma za afya vya vijiji vya Nhobora, Suzula na Itikilo mkoani Shinyanga, ambapo majengo ya vituo hivyo yaliharibika kabisa na kusababisha jamii kupata shida ya matibabu.
"Kuanzia sasa, serikali itahakikisha hospitali zote zitajengwa sehemu si hatarishi kama mabondeni ambazo juu ya milima mikali na kando ya bahari, aidha majengo yote yajengwe kwa kuzingatia viwango vya ujenzi ili yaweze kuhimili maafa," alisema.
Alisema wakati wananchi wa wanatafakari kuhusu suala zima la maafa, serikali itatekeleza kikamilifu mipango itakayohakikisha vyombo vya utoaji huduma za afya vinakingwa na majanga mbalimbali pamoja na kuwekwa katika sera ya nchi.
Maadhimisho hayo kitaifa yalifanyika katika viwanja vya Hospitali ya Temeke ambapo ujumbe wa mwaka huu unaeleza juu ya suala zima la usalama wa hospitali dhidi ya maafa kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu.
0 comments:
Post a Comment