
Wakazi wa Mbagala walioathirika na milipuko ya mabomu iliyotokea Aprili 26, mwaka huu katika kambi ya Jeshi la Wananchi, JWTZ leo wameanza kulipwa fedha zao za fidia.
Zoezi la kuwalipa wananchi hao limeanza saa 3:00 katika ofisi za Manispaa ya Temeke.
Alasiri ilipofika ofisini hapo, imeshuhudia wananchi hao wakiwa wamejipanda nje ya geti la manispaa hiyo.
Kutokana na wananchi wengi kudamkia kwenye ofisi hizo, askari Polisi na wale wa kampuni binafsi wanaolinda eneo hilo walikuwa na kazi ya ziada kuhakikisha watu wanaoingia ndani ya uzio ni wale tu wanaostahili kulipwa.
Akizungumza na Alasiri leo asubuhi, Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Bw. Said Mkumbo amesema, kwa mujibu wa ratiba waliyojiwekea, watakaolipwa leo ni wananchi zaidi ya 300 wanaoishi mtaa wa Mbagala Kuu.
Akasema wananchi wa mitaa mingine walioathirika leo hawahusiki kwenye zoezi hilo mpaka pale watakapotangaziwa kuwa zamu yao ya malipo imefika.
Pia amesema malipo yanafanyika kwa hundi na mhusika atatakiwa kwenda benki yoyote kupata fedha taslimu. Kwa wasio na akaunti benki, watatakiwa kufungua kwanza ndiyo wapewe hundi zao.
0 comments:
Post a Comment