Pichani ni Ndege aina ya Fokker 27
namba 5X-FFD ikiwa imeanguka ilipokuwa ikiajiandaa kuruka kutoka uwanja
wa ndege wa Wilson uliopo jijini Nairobi kutokana na hitilafu.
Na.Mwandishi wetu
Wakati Shirika la Ndege la
fly540 Tanzania likipanga kupanua wigo wa utoaji huduma katika maeneo
mbalimbali nchini baadhi ya abiria wamepata wasiwasi kuhusu usalama na
ubora wa ndege za abiria za shirika hilo.
Wasiwasi huo unafuatia ajali ya
moja ya ndege hizo iliyotokea Januari 28 mwaka huu jijini Nairobi, Kenya
ambapo ndege aina ya Fokker 27 namba 5X-FFD kuanguka ikiajiandaa kuruka
kutoka uwanja wa ndege wa Wilson uliopo jijini Nairobi kutokana na
hitilafu.
Mmoja wa wateja wa ndege za
shirika hilo ambalo awali lilijikita katika kusafirisha watalii katika
hifadhi zilizopo nchini na nje ya nchi amesema ingawa wamekuwa wakitumia
muda mfupi kwenda na kutoka Mwanza wanachohofia ni mfumo wa ukarabati
wa ndege hizo unavyoendeshwa.
Januari 24 mwaka huu fly540
lilizindua rasmi safari za ndege kati ya Dar es Salaam na jiji la Mwanza
ambapo itatoa huduma zake kila siku isipokuwa Jumamosi.
Mwishoni mwa Januari ndege ya
kampuni ya Fly540 ilianguka ikijaribu kupaa kwa majaribio katika shamba
la mahindi na mihogo lililo pembeni mwa uwanja wa ndege wa Wilson wakati
ikijiandaa kuruka.
Mmoja wa mashuhuda wa ajali hiyo
Bwana Albanus Kioko amesema ndege hiyo namba 5X-FFD ikiwa katika njia
ya kurukia ilianguka pembezoni mwa uzio wa uwanja na kutoa kelele kubwa
katika eneo hilo.
“Ilianza kuondoka vizuri, lakini
ilipofikia karibu na mwisho wa njia ya kurukia nilisikia muungurumo
kutoka katika moja ya injini zake na baadae kuanguka katika shamba hilo
la mahindi,” alisema Bwana Kioko.
Ripoti ya ajali iliyotolewa
inasema ndege hiyo iliyotengenezwa kwa muundo wa kubeba mizigo imeeleza
kwamba chanzo cha ajali hiyo ni moja ya injini zake kukosa nguvu wakati
ikitaka kuruka ambapo ilishindwa na kuanguka.
Aidha uchunguzi wa ajali hiyo
uliotolewa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ya Kenya (KCAA) kushindwa
huko kufanya kazi kwa moja ya injini za ndege ya kampuni ya Fly540 ndiko
kulikochangia ndege hiyo kushindwa kuruka.
Watu wanne waliokuwa kwenye
ndege hiyo ambao hawakujeruhiwa waliripotiwa kuchukuliwa hadi hospitali
ya Nairobi kwa ajili ya matibabu ingawa imeelezwa hadi sasa hali zao
zinaendelea vizuri.
Mkuu wa Polisi wa viwanja vya
ndege nchini humo James Mugera alisema uchunguzi zaidi kuhusiana na
ajali hiyo unaendelea na taarifa zaidi zinasema pengine ndege hiyo
ilishindwa kuruka baada ya tairi la mbele la ndege hiyo kupasuka
ikijiandaa kupaa.
Chanzo cha kuaminika kutoka
Uwanja wa ndege wa Wilson kimesema ndege 5X-FFD licha ya kufanyiwa
matengenezo haikutengemaa kwa ajili ya kuanza safari jambo lililochangia
kutokea kwa ajali hiyo.
Hii ni ajali ya pili kwa ndege
za kampuni ya Fly540 kutokea ikifuatiwa na ile ya ndege namba F27’s
iliyotokea mwaka 2009 wakati ikitua kwenye ardhi ya Somalia kama ndege
ya kukodishwa.
Ingawa mpaka sasa hakuna taarifa
zozote zinazoonesha kutokea kwa ajali kwa ndege ya abiria za kampuni ya
Fly540 wasiwasi unaongezeka kutokana na matukio hayo ya ajali za ndege
zinazopishana kwa kipindi cha miaka miwili tu.
Katika mazungumzo yao kuhusiana
na suala hilo wataalam wa mambo ya anga nchini Kenya wameshauri kitendo
hicho kutojitokeza tena katika njia ya kurukia kutoka na kuingia katika
kiwanja hicho cha ndege ambacho ni kikubwa na kinachozungukwa na makazi
ya watu.
Kutokana na tukio hilo wataalam
hao wamesema ajali za ndege za shirika hilo za mara kwa mara wanashauri
kuwepo na ukaguzi wa kitaalam wa uhakika kabla ya ndege za Fly540
hazijaruhusiwa kuruka kutoka katika kiwanja hicho.
Chanzo kingine cha habari kutoka
uwanjani hapo kimesema ili kulifanya eneo hilo kuwa salama kuna budi
kwa kiwanja cha ndege cha Wilson kutenganishwa na majengo, makazi ya
watu na majirani wanaokizunguka ili kuepuka madhara yanayoweza kutokea
kwa siku za usoni ajali kama hizo itakapotokea.
Alipotafutwa Meneja Uendeshaji
wa kampuni ya Fly540 Bwana Dickson Ooko ili kuzungumzia suala kwa njia
ya simu hakuweza kupatikana baada ya simu yake kutokuwa na majibu.

0 comments:
Post a Comment