
Padre wa Kanisa Katoliki Zanzibar, Lucian Malamsha amemsifu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Mohammed Seif Khatib kuwa anatekeleza kwa vitendo misingi juhudi za Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuwaletea maendeleo wananchi.
Padre Malamsha alitoa pongezi hizo jana katika kijiji cha Kiboje, Wilaya ya Kati Unguja baada ya Waziri Khatib kukabidhi nguzo 100 za umeme.
Alisema Nyerere aliwasogezea maendeleo wananchi bila ya kujali itikadi wala ukabila, mambo ambayo Waziri Khatib amekuwa akiyatekeleza kwa vitendo.
Alisema hatua ya kuwasogezea umeme wananchi ni ukombozi mkubwa kwa vile ndio njia pekee itakayoweza kuwasaidia kufanikisha miradi ya maendeleo na kupata huduma muhimu za kijamii.
Padre huyo, alisema ni viongozi wachache ambao wamekuwa karibu na wananchi na kutumia muda wao mwingi kutatua kero za wananchi.
“Kutokana na harakati nyingi alizonazo kuwatumikia wananchi, ndio maana Waziri Khatib amekuwa hanenepi na umbo lake limekuwa kama la Mwalimu Nyerere,” alisema.
Alisema binafsi alianza kumfahamu Khatib tangu alipokuwa kiongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na amekuwa miongoni mwa viongozi waadilifu na wanaofuata kwa vitendo misingi ya Nyerere.
“Nakuombeni wananchi wa jimbo la Uzini msiache mbachao kwa msala upitao, Waziri huyo mnamjua uwezo wake wa kutatua kero za wananchi na hasa zingatieni kuwa zimwi likujualo halikuli likakwisha,” alisisitiza Malamsha.
Khatib jana alikuwa katika ziara ya kukabidhi nguzo hizo na waya wa umeme wenye urefu wa mita 800 katika vijiji vya Mchangani, Bambi, Kiboje na Tunduni vya Jimbo la Uzini.
Akizungumza na wakazi wa vijiji hivyo, aliwataka kuachana na watu wanaochanganya dini na siasa kwa sababu wanaweza kuligawa taifa na kuondoa umoja na mshikamano.
0 comments:
Post a Comment