.jpg)
Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, wamefanikiwa kuwatia mbaroni watu watatu akiwemo mwanafunzi wa Chuo cha Biashara (CBE) wakiwa na vocha zenye thamani ya Sh. milioni 90 za kampuni ya simu za mkononi Vodacom zinazosadikiwa kuwa ni za wizi.
Kamanda wa polisi wa kanda hiyo, Suleiman Kova alisema jana kuwa, watuhumiwa hao waliwakamata wiki hii katika viwanja vya Leaders Club wakati wakiwa katika harakati za kuziuza kwa Sh. milioni 45 badala ya Milioni 90.
Kamanda Kova alisema vocha hizo zilikuwa ni za Sh. 10,000 na Sh. 5000.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Muhsini Amin (21) ambaye ni mwanafunzi wa CBE, Sadick Jediwa (21) mkazi wa Tandale na Rashidi Maulidi (28) anayeishi Mwananyamala.
Alisema baada ya kupata taarifa juu ya watu hao mtego uliwekwa eneo hilo na kufanikiwa kuwakamata.
"Tulimtuma mtu ajifanye kama mteja na baada ya kufika pale, walikubali kuziuza vocha zote kwa Sh. milioni 45 badala ya Sh. milioni 90," alisema
Kamanda Kova alisema uchunguzi wa awali umebaini kuwa watu hao sio mawakala wa kampuni hiyo ya Vodacom.
Alisema kukutwa na vocha zenye thamani hiyo kunaonyesha wazi kuwa walizipata isivyo halali.
Alisema uchunguzi zaidi unaendelea ikiwa ni pamoja na kuwahoji wapi wamezipata.
0 comments:
Post a Comment