
Bodi ya mikopo imepiga mkwara wale wote wanaogushi vyeti ili kujipatia mikopo ya elimu ya juu kutoka katika bodi hiyo na kusema kuwa wataokaothubutu kufanya hivyo mwaka huu watakiona chamoto.
Akizungumza na Alasiri, Afisa Habari wa bodi hiyo, Bw. Cosmas Mwasobwa, amesema tangu Serikali iweke viwango vya ufaulu ili kupata mikopo, kumekuwa na baadhi ya watu wanaogushi vyeti ili kuidanganya bodi kwa lengo la kupata mikopo kwa ajili ya elimu ya juu.
"Hakuna cheti cha kughushi kinachoweza kumfanya mtu apate mkopo... hata kama kimetengenezwa wapi. Uhakiki wetu ni makini na wa kisasa," akasema.
"Na ndio maana tumekuwa kila mwaka tukiwakamata wale wote wanaojaribu kuwasilisha vyeti feki," akaongeza.
Akaongeza kuwa licha ya njia za kitalaamu wanazotumia sasa kugundua na kuwanasa wale wote wanaogushi vyeti, pia ofisi yake imekuwa ikishirikiana kwa karibu na wenzao wa Baraza la Mitihani nchini, NECTA ili kuhakiki vyeti hivyo.
Mathalan, akasema katika ushirikiano huo, ofisi yake imeweza kuwa na vitabu vya matokeo vya baraza la mitihani ya miaka yote ili kujua usahihi wa vyeti vinavyowasilishwa katika bodi hiyo na hivyo haiwapi shida kuwabaini wadanganyifu.
0 comments:
Post a Comment