
Rais Jakaya Kikwete aliondoka nchini jana jioni kuelekea New York, Marekani kuhudhuria kikao cha 64 cha Baraza la Umoja wa Mataifa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Ikulu jana jioni, Rais Kikwete anatarajiwa kuhutubia baraza hilo Alhamisi ambapo ufunguzi rasmi utafanyika Jumatano.
Mbali na kuhutubia Baraza Kuu la UN, Rais Kikwete anatarajiwa kuhudhuria mikutano mbalimbali iliyoandaliwa na UN kwa ajili ya viongozi wakuu wa nchi watakaokuwepo mjini New York.
Baadhi ya mikutano hiyo ni mkutano wa mabadiliko ya hali ya hewa unaoandaliwa na Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-Moon. Mkutano huo ni mmoja wa mikutano ya maandalizi kuelekea mkutano mkuu wa hali ya Hewa Duniani utakaohudhuriwa na viongozi wakuu duniani huko Copenhagen, Denmark Desemba mwaka huu ambapo mkataba mpya wa kukabiliana na tishio la mabadiliko ya tabia nchi utapitishwa.
Rais pia atahudhuria kikao cha uzinduzi wa mpango wa pamoja wa viongozi wa Afrika kupambana na malaria barani, Africa Leaders Malaria Alliance (ALMA), ambapo Tanzania ni mwenyekiti mwenza na imeshirikiana na UN kuandaa mkutano huu. Rais Kikwete na Mshauri maalum wa UN, Ray Chambers wataongoza kikao hicho.
Katika kikao kingine, Rais Kikwete pamoja na Waziri Mkuu wa Uingereza, Gordon Brown kwa pamoja wataongoza kikao cha viongozi kuzungumzia malengo ya milenia namba 4 na 5, malengo yanayohusu kupunguza vifo vya watoto wachanga na mama wajawazito. Rais wa Marekani, Barack Obama, amewaalika viongozi wa Afrika kwa ajili ya chakula cha mchana ambapo Rais Kikwete anatarajiwa kutambulisha mada muhimu juu ya kuimarisha Kilimo na jinsi kinavyoweza kuchagiza nafasi za kiuchumi barani Afrika.
Rais pia anatarajia kukutana na viongozi kadhaa, wafanyabiashara na wawekezaji. Atafungua jengo la Ubalozi wa Tanzania jijini Washington na kurejea nyumbani Oktoba Mosi.
1 comments:
Aaaaahhhh!!! Vasco Da Gama wangu kama kawa.
Tambaa mkuu wangu
Post a Comment