
Walaji wa nyama katika mji wa Tunduma wilayani Mbozi mkoani hapa wamewatupia lawama viongozi wa Mamlaka ya mji huo pamoja na Umoja wa Wauzaji wa Nyama ya Ng'ombe (Uwanyatu) kutokana na kuruhusu kupanda kwa bei kiholela hali iliyosababisha watu wenye kipato cha chini kushindwa kumudu.
Wakizungumza na Nipashe jana, walisema viongozi wameshindwa kuchukua hatua dhidi ya Umoja wa Wauzaji wa Nyama ya Ng'ombe ambao wamekuwa wakipandisha bei bila kujali athari wanazopata wanananchi.
Mmoja wa wakazi hao, Songolo Tozo, alisema tangu Agosti 7, mwaka huu, Uwanyatu umetangaza kupandisha bei ya nyama kutoka sh.3000 na kufikia sh.3,800 kwa kilo moja.
Tozo alisema tangu kupanda kwa bei hiyo ambako kumesababisha baadhi ya wananchi wenye kipato cha chini kushindwa kununua nyama, katika hali ya kushangaza viongozi wa Mamlaka ya mji wa Tunduma wamekaa kimya na hivyo wananchi kuhisi kuwa huenda wamekubaliana na ongezeko hilo la nyama.
Walaji hao walisema sababu zilizotolewa na Uwanyatu kwamba wamepandisha bei ya nyama kutokana na kupanda kwa gharama za usafirishaji wa ng'ombe kwenda kwenye machinjio mapya hazina msingi kwa kuwa awali machinjio yalipokuwepo hakuna umbali wa zaidi ya kilometa tatu.
Ofisa Mtendaji wa Mamlaka ya Mji wa Tunduma, Aidan Mwashiga, akijibu malalamiko hayo alisema lawama za kupandishwa kwa bei ya nyama zinapaswa kuelekezwa kwa viongozi wa Uwanyatu kwa sababu mchakato wa kuongeza bei hiyo mamlaka haikushirikishwa.
Mwashinga alisema kigezo kilichotumiwa na viongozi hao kupandisha bei ya nyama kutokana na kupanda kwa gharama ya usafirishaji wa ng'ombe kwenda kwenye machinjio, siyo sababu ya msingi kwa sababu machinjio mapya yalipojengwa hakuna umbali wa zaidi ya kilometa tatu kutoka katika machinjio ya zamani.
0 comments:
Post a Comment