SERIKALI imetahadharisha juu ya uwezekano wa kuwepo kwa mvua kubwa za El Nino, katika maeneo mengi ya nchini katika kipindi cha kati ya Oktoba na Desemba mwaka huu.
Tahadhari hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Philipo Marmo, alipokuwa akifungua mkutano wa maandalizi ya kukabiliana na mvua hizo.
Alisema utafiti uliofanywa na mamlaka ya hali ya hewa katika nchi mbalimbali, umeonyesha kuwa Tanzania itakumbwa na mvua hizo kwa kiasi kikubwa.
“Asilimia 60 ya nchi, kwa sasa ina ukame kwa hivyo El Nino inaweza kuwa na manufaa kama wananchi watajiandaa vizuri,”alisema Marmo.
Waziri Marmo alisema madhara ya El Nino ni makubwa ikiwa ni pamoja na uharibifu wa miundombinu, skimu za umwagiliaji, mazao, magonjwa ya milipuko na homa ya Bonde la Ufa.
Hata hivyo alisema athari za El Nino hutofautiana kutoka sehemu moja hadi nyingine na kwamba utafiti huo umeonyesha El Nino ya mwaka huu, itaathiri zaidi Mkoa wa Dar es Salaam, Mashariki na Kaskazini.
Alisema mkutano huo ambao ni wa kwanza kufanyika kwa ajili ya maandalizi ya mvua hizo, umewahusisha maofisa Idara ya Maafa, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), mikoa na wilaya zitakazoguswa na mvua hizo na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali.
Waziri huyo alitoa wito kwa viongozi wa ngazi mbalimbali kuwaelimisha wananchi, kuhusu madhara ya mvua hizo hasa wakazi wanaoishi maeneo ya mabondeni.
Kwa upande wake mwakilishi wa UNICEF, Mohamed Safieldin, aliviomba vyombo vya habari kutoa elimu kwa umma kuhusu athari za mvua za El Nino.
0 comments:
Post a Comment