Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dk. Abeid Amani Karume, amewashauri akina mama nchini kuwahamasisha akina baba ili nao waitumie kikamilifu benki yao ya Wanawake nchini.
Ushauri huo ameutoa Jijini wakati akifungua mafunzo ya wanawake wajasiriamali kwenye ukumbi wa Mhasibu Jijini.
Rais Karume akasema kuwa wanawake wamepata bahati kwakuwa mkombozi wa mtaji wao amekwishaingia nchini, hivyo watumie nafasi hiyo kuwahamasisha akina baba nao wajiunge na benki hiyo.
"Kwa bahati nzuri, mkombozi wa mtaji kwa wanawake wote nchini tayari anakuja. Naye ni Benki ya Wanawake Tanzania, baada ya matayarisho ya muda mrefu... nawashauri muwahamasishe akina baba nao waitumie kikamilifu benki hiyo," akasema Rais Karume.
Aidha, akatoa wito kwa wajasiriamali wanawake kuitumia vyema benki hiyo kwa kuweka akiba zao na kupata mitaji ya kufanyia biashara.
Katika hatua nyingine, Rais Karume akawahimiza wanawake kupima afya zao.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mfuko wa Fursa sawa kwa wote (EOTF), Mama Anna Mkapa, akizungumza katika mkutano huo, akasema kuwa umaskini haukubaliki bali unakwepeka, hivyo changamoto iliyopo ni ya wake kwa waume, tena kuanzia ngazi ya kaya hadi Taifa.
"Kwa mantiki hiyo mfuko wa fursa sawa kwa wote, umeivalia njuga changamoto hiyo kwa kwenda kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wanawake katika ngazi ya vijiji, wilaya na mikoa iliyoko pembezoni mwa nchi yetu ambayo haijafikiwa na watu wengi katika ukombozi wa mwanamke," akasema Mama Mkapa.
0 comments:
Post a Comment