Dereva wa pikipiki al maaruf "bodaboda", Juma Rashidi, 32, mkazi wa
Itigi wilayani Manyoni mkoani Singida ameuawa na abiria aliyekuwa
anamsafirisha kwenda kijiji cha Tura mkoani Tabora.
Kamanda wa
jeshi la polisi mkoani Singida Celina Kaluba amesema dereva huyo
alikatwa kisogoni na kitu chenye ncha kali na abiria huyo Geu Njongaji
na kudondoka chini kisha kuchinjwa shingo.
Mtuhumiwa Geu baada ya
kufanikisha mauaji hayo alipora pikipiki yenye namba za usajili T 962
BNF aina ya Sanlag na kukimbia nayo kuelekea kwao kijiji cha Tura. Akiwa
anaendesha pikipiki hiyo kwa mwendo wa kasi hakufika mbali kabla ya
kugonga shina la mti mkubwa na kuumia vibaya. Akaamua kurudi Itigi kwa
ajili ya kupata matibabu katika hospitali ya misheni ya St.
Gasper. Wananchi waliokuwa wameshapata taarifa ya dereva wa bodaboda
kuuawa walipomwona, walimvamia na kuanza kumpiga.
Geu aliweza
kupenya na kuwatoroka kwa kukimbilia katika chumba cha walinzi wa benki
ya NMB Itigi kwa lengo la kujisalimisha. Wananchi wakawashinikiza Askari
waliokuwa lindoni wamtoe Geu lakini Askari hao hawakukubaliana na ombi
lao. Ndipo wananchi walipofanya fujo kubwa na kuharibu milango,
madirisha na vioo vya magari na kufanikiwa kumtoa Geu ambapo walimpiga
kwa silaha mbalimbali hadi alipokata uhai. Kamanda Kaluba amesema
polisi inawashikilia Mohammed Masoud (24) na David Nicodemo
(25)kuhusiana na mauaji hayo na kuharibu mali ya benki.
|
0 comments:
Post a Comment