Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu (CCM) ni miongoni mwa waliotoa tahadhari ya udini.
* Mmoja asema serikali kuanzisha taasisi za dini ni kuvunja katiba
Exuper Kachenje, Dar na Kizitto Noya, Dodoma
HOJA ya Tanzania kujiunga na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kiislamu (OIC) na mijadala mingine ya dini imezidi kuwa moto baada ya wabunge watatu kuionya serikali kuwa masuala hayo yataigawa nchi katika vipande vipande.
Waliotoa onyo hilo ni pamoja na Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu (CCM), Mbunge wa Maswa (CCM), John Shibuda na yule wa Bukene (CCM) Teddy Kasela-Bantu walipokuwa wakichangia hotuba ya makadirio, mapato na matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa iliyowasilishwa na Waziri Bernard Membe.
Aliyekwenda mbali zaidi ni Nyalandu aliyetangaza nia ya kuwasilisha muswada binafsi kulitaka bunge kuzuia mjadala wa suala lolote la dini.
Kauli hizo zimekuja katika kipindi ambacho taifa limeshuhudia mijadala mikali inayochukua sura ya kidini, kuhusiana na uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi Tanzania Bara, nchi kujiunga na OIC na waraka wa Wakatoliki unaoelekeza Watanzania namna ya kupata viongozi bora katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Nyalandu aliitahadharisha serikali kuwa hatua yoyote ya kushiriki katika uanzishwaji wa mamlaka au taasisi yoyote ya dini nchini ni uvunjaji wa katiba ya nchi na inaweza kuligawa taifa.
Huku akipinga kuendelea kwa mjadala wa Tanzania kujiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu (OIC); na kutoa mifano mbalimbali ya mataifa yaliyofuata misingi ya dini na athari zake na kunukuu vifungu vya Katiba ya Tanzania, Nyalandu alisema serikali ya Tanzania haina dini na hivyo haina mamlaka ya kusimamia uanzishwaji wa taasisi au mamlaka yoyote ya kidini.
“Itakuwaje tuanze kujadili masuala ya dini katika nchi ambayo haiongozwi kwa misingi ya dini?” alihoji Nyalandu na kuongeza:
“Serikali kimsingi hairuhusiwi kuwa na dini, lakini pia hairuhusiwi kusaidia uanzishwaji wa chombo chochote au mamlaka yoyote, yenye misingi ya dini ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.”
Aliongeza kuwa, “haitakuwa jambo la busara na itakuwa ni kukiuka misingi ya katiba ya nchi, kuruhusu aina yoyote ya michakato inayohusu masuala ya dini moja dhidi ya dini nyingine.”
Nyalandu alimkumbuka Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere alipokataa lilipoibuka suala la Zanzibar kujiunga na OIC.
Alisema suala jingine linalofanana na hilo ni la uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi au nyingine yoyote inayofanana na hiyo na kueleza kuwa, pia litakuwa ni uvunjaji wa katiba iwapo litajadiliwa bungeni.
“Suala la dini ni nyeti sana, nchi hii ilikaa na watu wa dini zote. Dini au kabila vitaligawa nchi vipande. Tumeona ukabila ukiitafuna Kenya na sasa udini umeanza kuingia Tanzania,” alisema Nyalandu na kuendelea:
“Katika hilo, nakusudia kuleta muswada binafsi kupiga marufuku Bunge kujadili mambo ya dini na matumizi ya fedha za walipakodi katika kusaidia uanzishwaji wa taasisi yoyote ya dini hapa nchini,” alisema.
Aliendelea, “Ninaonya wanasiasa kunyemelea masuala ya dini na kuyajadili bungeni, wakuu wa dini kutaka mambo yao yaje kwenye siasa. Tufute kabisa kujadili OIC, hili ni shirika lao huko. Hakuna mchakato hapa, Tanzania sio nchi ya dini.”
Msimamo wa Nyalandu kupinga OIC, uliungwa mkono kwa nyakati tofauti na mbunge wa Maswa (CCM), John Shibuda na Mbunge wa Bukene (CCM) Teddy Kasela-Bantu waliosema kuwa, kufanya hivyo, ni kukiuka Katiba na misingi iliyowekwa na waasisi wa Tanzania akiwamo Mwalimu Julius Nyerere.
“Wabunge turejee na kufuata matakwa ya katiba tuliyoapa kuilinda, hifadhi ya amani ya Tanzania inategemea maneno yetu sisi wabunge, tuzungumze kwa masilahi ya Taifa,” alisema Shibuda na kuonya:
“Tusitumie lugha za tafrani, tusiwe wanaharakati wa dini hapa bungeni. Tusiwe ndondondo za tafrani kwa nchi yetu, tusiwe misumari ya jeneza la amani ya Tanzania, tukumbuke hakuna atakayetawala kwa kutegemea dini moja.”
Naye Mbunge wa Bukene, Teddy Kasela- Bantu aliwataka wabunge kuendelea kuitetea Katiba ya nchi akionya kuwa endapo viongozi wakianza kuivunja kwa makusudi, nchi itasambaratika.
“Kama viongozi tunaivunja Katiba tuliyoapa kuitetea, wananchi wafanya nini?” alihoji Kasela- Bantu na kuendelea, “Katiba inasema serikali haina dini, sasa kama humo ndani tunaanza kuzungumzia mambo ya dini ni wazi tunavunja katiba.”
“Mimi naomba hata kama mchakato wao huo utachukua miaka mingapi, Tanzania tuache kufikiria jambo hilo la kujiunga na OIC. Kila mtu anatakiwa kuamini anachoamini, cha Kaisari tumpe Kaisari ambaye ni serikali na cha roho kibaki rohoni, nchi hii haina dini,” alisisitiza.
Awali, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe aliwataka Watanzania wasitishe kwa muda mjadala wa Tanzania kujiunga na Jumuiya hiyo kwa kuwa OIC sasa ipo kwenye mchakato wa kubadilisha sheria na kanuni zake za namna ya kupata wanachama wapya.
“OIC ipo kwenye reform ya kuundwa upya, inafanyiwa mabadiliko ya muundo, taratibu, kanuni za kuwapata wanachama wapya. Naomba Bunge na Watanzania kuelewa mabadiliko hayo ili mjadala huu usitishwe hadi mwaka 2012 utakapokamilika mchakato huo,” alisema Membe na kuendelea.
“Hatuwezi kuendelea na mjadala wakati chombo chenyewe kinapitia mfumo na mabadiliko katika kipindi cha miaka miwili ijayo. Tukiendelea kujadili, tutakuwa tunajadili mambo yatakayopitwa na wakati. Haya sio maneno ya Membe, ni maelekezo ya kikao cha OIC kilichoketi mjini Damascus, Syria mwezi Mei mwaka huu.”
Membe alibainisha kuwa mchakato huo unafanywa na nchi nne ambazo zitatakiwa kumaliza kazi mwaka 2010 na kutoa taarifa yake kwenye baraza la wataalamu wa OIC mwaka 2011 kabla ya kufikisha taarifa kwa nchi wanachama.
Akieleza hasara za nchi kujiingiza katika masuala ya dini, Nyalandu alisema, machafuko yaliyotokea Zambia katika siku za hivi karibuni na mapigano ya Kitaleban nchini Pakistan ni matokeo ya uamuzi huo ambao Tanzania inataka kuufanya.
Hoja ya Nyalandu kwamba wanawake wa Saud Arabia wanakatazwa kuendesha magari kutokana na tamaduni za dini zao iligusa hisia za mbunge wa Mchinga (CCM) Mudhihir Mudhihir ambaye alisimama na kuomba mwongozo wa Naibu Spika akisema:
“Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mheshimiwa mbunge afute kauli yake kwamba dini ya Uislamu inakataza wanawake kuendesha magari ili asiamshe jazba zetu.”
Hata hivyo, Naibu Spika Anne Makinda alipuuza mwongozo huo akisema, “Mimi naamini mheshimiwa hakutaja dini, alisema Uingereza ukioa mke wa pili unafungwa; na Saud Arabia wanawake wanakatazwa kuendesha magari kwa mujibu wa tamaduni na dini zao,” alifafanua Makinda na kuomba Hansard kuthibitisha kauli yake.
Akihitimisha mjadala wa hotuba ya bajeti yake, Waziri Membe alisema serikali itaendelea kutokuwa na dini (secular state) huku akifafanua kuwa, “Si kwamba serikali inataka kuondoka katika “secular state” bali OIC inataka serikali za nchi kuwa wanachama na si taasisi, lazima serikali itoe kibali ndipo nchi iwe mwanachama, lazima tuwe na `tolerance` (tuvumilie).
Wakati hayo yakijadiliwa ndani ya Bunge, nje ya Bunge huko huko Dodoma, Habel Chidawali anaripoti kuwa, Waislamu mkoani humo wamesema kuwa wamechoka na kitendo cha serikali kuwadanganya kama watoto wadogo na sasa wanataka Mahakama ya Kadhi kwa nguvu zote.
Kauli hiyo waliitoa jana wakati wa kongamano la Waislamu wa mkoa huu lililofanyika katika Ukumbi wa Maktaba mjini chini ya udhamini wa shirika lisilo la kiserikali la Al-Mallid la mjini humo.
Waislamu hao walisema kuwa umefika wakati ambao wanaamini kuwa serikali inatoa haki kwa upendeleo kwa kuwajali zaidi Wakristo huku masilahi ya Waislamu yakisahaulika kabisa.
0 comments:
Post a Comment