amadhan Semtawa
BODI ya Wakurugenzi ya Shirika la Fedha la Ulimwenguni (IMF) , kupitia mpango maalum (Special drawing-SDR) utaipatia Tanzania dola za Marekani 230 milioni, ili kutunisha hazina ya fedha za kigeni.
Taarifa zilizopatikana zinaeleza kwamba bodi ya IMF, imekuwa na mazungumzo na Tanzania kwa muda wa mwezi mzima sasa.
Gavana wa BoT alipoulizwa katika mahojiano maalumu yaliyofanyika ofisini kwake jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, alithibitisha kufanyika mazungumzo hayo.
"Kwa mazungumzo ni kweli tumekuwa tukizungumza, lakini suala la kutolewa fedha, wao wataamua," alifafanua Gavana Profesa Ndulu.
Alipoulizwa zaidi kuhusu mpango huo wa SDR, alisema ni kweli upo na Tanzania kama mwanachama wa IMF inaweza kunufaika nao.
"Lakini, hilo la kutoa fedha wao wenyewe, wataamua, kama zipo subirini, mtaambiwa siku ikifika, ila sasa hivi bado sina taarifa za maamuzi," alisisitiza gavana.
Hata hivyo, Gavana akikataa kuthibitisha taarifa zinaonyesha bodi ya IMF na ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na watendaji wa BoT ilikubaliana katika mazungumzo yao yaliyofanyika Marekani hivi karibuni kutoa kiasi hicho kama mkopo.
Tayari IMF wakati wa mwanzo wa mtikisiko wa uchumi ilitoa kiasi cha dola 300 milioni, kusaidia hazina ya fedha za kigeni za Tanzania.
Katika mazungumzo hayo, Tanzania itapata dola za Marekani 230 milioni kwa lengo la kutunisha zaidi hazina ya Fedha za Kigeni (Foreign Exchange).
Duru hizo za kimtandao zilionyesha kwamba, kiasi hicho cha fedha huenda kikatolewa wakati wowote kuanzia mwezi ujao.
Tanzania ni moja ya nchi ambazo zimeathirika na mtikisiko wa uchumi wa dunia kwani hivi karibuni Kikosi Kazi (Task Force), chini ya gavana Ndulu kilitoa ripoti yake ambayo ilimfanya Rais Jakaya Kikwete kutangaza mpango mkubwa wa kunusuru uchumi wa Sh 1.7trilioni.
0 comments:
Post a Comment