
Mjumbe Mitchell and waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesema walikuwa na mazungumzo yaliokuwa na mtazamo mzuri unaonuia kuanzisha tena utaratibu wa amani wa Mashariki ya Kati.
Suala la Israel kusimamisha ujenzi wake katika maeneo ya Wapalestina halikutajwa japo Marekani imekuwa inadai ujenzi huo usitishwe mara moja.
Bw. Mitchell ni mmoja wa maafisa wakuu wa Marekani katika eneo hilo wanaojaribu kushughulikia mpango wa amani wa Mashariki ya Kati.
Wapalestina kwa upande wao wamesema ujenzi wote wa Israel katika maeneo yaliokaliwa kimabavu lazima ukomeshwe kabla ya mazungumzo kuanza.
Uhusiano mbaya
Baada ya mkutano uliochukuwa karibu saa tatu uliotarajiwa kuangazia zaidi suala la makazi, mabwana hao wawili walizungumza na waandishi wa habari kwa kifupi. Suala la Ujenzi halikutajwa kamwe.
Bw. Netanyahu alisema wanapiga hatua kuh usu kuafikia maelewano yatakayo wawezesha kuendelea na kukamilisha utaratibu wa amani kati ya majirani wa Palestina na nchi nyengine katika eneo hilo .
Uhusiano kati ya maswahiba hawa wawili ulionekana kutikisika kidogo katika wiki za hivi karibuni baada ya Marekani kudai ujenzi unaofanywa na Israel katika maeneo yanayokaliwa kimabavu ukomeshwe mara moja.
Marekani inatilia mkazo hatua za kidiplomasia katika kuafikia mpango madhubuti wa amani ya Mashariki ya Kati. Mshauri wa kitaifa wa Rais Barack Obama James Jones na mwanadiplomasia Dennis Ross pia wanatarajiwa kuwasili katika eneo hilo kuchangia katika juhudi hizo za kuleta amani.
Awali, mjumbe Mitchell alimwambia Rais wa Israel Shimon Peres kwamba Israel inaweza kuimarisha hali ilivyo sasa kwa kukabiliana na masuala nyeti kama vile ujenzi wa makazi ya Israel katika maeneo yaliokaliwa na vile vile vituo vya ukaguzi kuingia na kutoka maeneo ya wapalestina.
0 comments:
Post a Comment